Tuesday, April 29, 2014

Ushirikiano huu wa ‘Ukawa’ uwe endelevu

mboye_a034a.jpg
Bila shaka kila mwananchi anayeitakia mema nchi yetu amevutiwa na habari zilizochapishwa katika gazeti hili jana kwamba vyama vya siasa vinavyounda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa), vimeamua kushirikiana katika Uchaguzi Mkuu wa 2015 kwa kusimamisha mgombea mmoja katika nafasi ya urais, ubunge na udiwani.
Viongozi wakuu wa vyama hivyo tayari wamekubaliana kuanza mchakato huo na wameandika mapendekezo na kuyapeleka katika sekretarieti za vyama vyao kwa ajili ya kufanyiwa uchambuzi.
Sisi tunaona kitendo hicho cha vyama vinavyounda Ukawa kuwa ni hatua muhimu ya kuongeza nguvu ili kuongeza ushindani ambao ni muhimu katika mustakabali wa nchi yetu kisiasa na hivyo kusaidia nyanja nyingine za kiuchumi na kijamii.
Tangu kuruhusiwa tena kwa siasa huru karibu miaka 22 sasa, bado nchi haijashuhudia ushindani wa kweli unaoweza kuwafanya watawala kuwajibika kwa wananchi kutokana na kuona hatari ya kuondolewa madarakani na vyama pinzani.
Hii imetokana na vyama shindani katika siasa kukumbwa na mifarakano ya kisiasa ambayo imekuwa ikiwagawa na hivyo kuingia kwenye chaguzi vikiwa dhaifu na hivyo kushindwa vibaya na chama tawala na matokeo yake yamekuwa ni wananchi wengi kukata tamaa na hivyo kusababisha idadi ya wanaoshiriki kupiga kura kupungua mwaka hadi mwaka kutokana na kutoona faida ya siasa za ushindani.
Pengine hiyo ndiyo sababu iliyofanya wananchi wapendekeze kwa Tume ya Mabadiliko ya Katiba kwamba vyama viruhusiwe kuunganisha nguvu wakati wa chaguzi kwa kuwa wameona bila ya nguvu ya vyama shindani, watawala wawataendelea kuongoza kwa mazoea na matokeo yake ni wananchi kuendelea na umaskini wao na kuona uhuru wa vyama vya kisiasa hausaidii kuwa kuboresha maisha yao.
Si nia yetu kuona chama tawala kikiondolewa madarakani na vyama shindani, lakini tunachotaka kuona na ushindani wa dhati, makini na wa kweli ambao, kwa taifa lolote lile, ni afya kwa ustawi wa wa taifa kwa kuwa huongeza uwajibikaji kwa watawala.
Hakuna ubishi kwamba upinzani wenye nguvu huisukuma serikali ichape kazi na kuwatumikia wananchi kwa kutambua kwamba ikiboronga itaondolewa madarakani na serikali kivuli ambayo ni vyama vya upinzani.
Vyama legelege vya upinzani huogopa kivuli cha serikali na kufifisha maendeleo na kuzima matumaini ya wananchi wanaotaka kuona uwajibikaji serikalini, kwani huwa chachu ya kuendeleza tawala za kiimla zisizothamini demokrasia na zisizowajibika kwa wananchi.
Ndiyo maana tunawapongeza viongozi wa Ukawa kwa kuona umuhimu wa kuunganisha nguvu na kuwa wamoja ili kuweka ushindani wa kweli katika mazingira ya kisiasa tuliyomo.
Tunachoweza kuwashauri viongozi wa Ukawa ni kuwa makini na kuondoa tofauti zinazowatenganisha. Ukawa isitarajie kwamba kila kitu kitakuwa mteremko, kwani bado sheria kandamizi ambazo zimekuwa zikikwaza shughuli za upinzani bado hazijafutwa.
Ni matarajio yetu kwamba serikali na chama tawala kitachukulia hatua hiyo ya Ukawa kuwa changamoto ya kuongeza ufanisi katika kuwatumikia wananchi na si kuanza kujenga chuki na kutafuta mbinu za kuikwamisha
Serikali haina budi kuhakikisha kuwa vyama vyote vinapewa nafasi sawa ya ushindani na kujengewa mazingira ya kukua ili kukifanya chama chochote kinachopewa madaraka kiwajibike kwa wananchi na kuwaletea maendeleo.(E.L)

source: mjengwa blog

Breaking News: Azam FC wakamilisha usajili wa Kavumbagu


KAVUMBAGUNEW_43297.jpg
Klabu ya Azam FC imeanza rasmi maandalizi ya kutetea ubingwa wao msimu ujao na michuano ya kimataifa kwa kukamilisha usajili wa mchezaji wa kimataifa wa Burundi aliyekuwa anakipiga kwenye klabu ya Yanga.
Taarifa rasmi zilizothibitishwa na meneja wa Azam FC Jemedari Said ni kwamba mshambuliaji Didier Kavumbagu amejiunga na klabu hiyo kwa mkataba wa mwaka mmoja.
“Ni kweli Kavumbagu tumemalizana nae na amesaini mkataba wa mwaka mmoja. Taarifa zaidi zitatolewa baadae.” Alikaririwa Jemedari.
Kavumbagu alitua nchini Tanzania akitokea Burundi alipokuwa anaitumikia Vital O na kuja kujiunga na Yanga misimu miwili iliyopita.(Awadh Ibrahim)
 
source: mjengwa blog

Basi la Hood lilivyoungua moto na kuteketea kabisa



Zaidi ya Abiria 55 waliokuwa ndani ya Basi la kampuni ya Hood, wakisafiri kutoka Mbeya kwenda Arusha walinusurika kufa baada ya Basi hilo kushika moto na kuteketea kabisa katika kijiji cha Kilolele-Chalinze Mkoani Pwani.Chanzo: http://bit.ly/1m4F9cG (J M)

source: mjengwa blog

Sunday, April 27, 2014

Sherehe zatikisa Dar

  Makomandoo wa jeshi wawa kivutio
  Askari wa Miavuli wapongezwa
  Wapinzani wasusia Sherehe
Askari wa miavuli akishuka na parachuti kwenye Uwanja wa Uhruru wakati wa sherehe za miaka 50 ya Muungano wa Tanganyika na Zanzibar jijini Dar es Salaam jana.
Sherehe za miaka 50 ya Muungano jana zilifana na kusababisha viwanja vya Uhuru na Taifa kufurika umati wa watu waliojitokeza kuungana na viongozi wa kitaifa na kimataifa kusherehekea maadhimisho hayo.
Uwanja wa Uhuru ambao ulitengwa kutumika kwa ajili ya sherehe hizo, baada ya kujaa askari walilazimika kufungua lango kuu la kuingilia Uwanja wa Taifa, ili wananchi waliokuwa nje waingie kushuhudia yaliyokuwa yakiendelea uwanja wa Uhuru.

Wananchi wengine walilazimika kukaa nje ili kufuatilia sherehei za Muungano kupitia televisheni iliyokuwa imefungwa nje ya viwanja.

Mageti ya uwanja wa Uhuru yalikuwa wazi kuanzia saa 12:30 asubuhi na ilipofikia saa 2:30 viongozi mbalimbali wa ngazi tofauti ndani na nje ya nchi walianza kuingia.

Sherehe hizo  zilihudhuriwa na marais sita wa kimataifa, akiwemo Mfalme wa Lesotho Letsie III, Mfamle wa Swaziland Mswati III,  Rais wa Uganda, Yoweri Museveni, Rais wa Burundi,  Pierre Nkurunzinza, Rais wa Malawi, Joyce Banda na Rais wa Kenya, Uhuru Kenyatta.

Pia zilihudhuriwa na marais wastaafu wa ndani na nje ya nchi akiwemo Sam Nujoma (Namibia), Rupia Banda (Zambia) na Mwai Kibaki (Kenya).

Rais mstaafu wa Awamu ya Tatu, Benjamin Mkapa ni miongoni mwa viongozi waliohudhuria sherehe hizo.

Wawakilishi wa nchi, mashirika ya kimataifa pamoja na mabalozi na viongozi wengine wa kitaifa waliohudhuria ni Waziri Mkuu mstaafu Edward Lowassa, Spika wa Baraza la Wawakilishi Zanzibar, Pandu Amir Kificho na Katibu Mkuu wa CCM, Abdulrahaman  Kinana.

Pia maadhimisho hayo yalihudhuriwa na wawakilishi kutoka nchi za Oman , Angola, Kuwait, Mauritius, Botswana, Ghana, Jamaica, Ufaransa , Korea Kusini, Brazil, Uholanzi, Finland Uingereza, Qatar, Eritrea, Misri na Algeria.

Hata hivyo, baadhi ya viongozi wa vyama vya siasa vya upinzani walionekana kususia sherehe hizo kwa kutoonekana uwanjani hapo.

Viongozi hao ni Mwenyekiti wa Chadema, Freeman Mbowe,  Mwenyekiti wa NCCR-Mageuzi, James Mbatia, Mwenyekiti wa CUF, Profesa Ibrahim Lipumba ambao wanaunda kundi la Umoja wa Katiba ya Wananchi (UKAWA).

Viongozi ambao walianza ni Spika wa Bunge, Anne Makinda akifuatiwa na makatibu wakuu, Rais Mstaafu wa Zanzibar, Abeid Karume, Rais mstaafu wa awamu ya tatu, Benjamin Mkapa  kisha akafuatia mke wa marehemu Abeid Karume, Fatma.

Haikupita muda, aliingia  Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar, balozi Seif Ali Iddi, na kufuatiwa na makamu wa Kwanza wa Rais Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad,  jukwaa kuu eneo walikokaa mawaziri na wabunge, walisikika wakisema, mbili yatosha tatu ya nini, CCM yatosha.

Ilipotimu saa 3:20 Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, aliwasili akifuatiwa na mawaziri kutoka nchi mbalimbali kisha Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein aliingia.

Makamu wa Rais, Dk. Mohammed Gharib Bilal kisha Rais Mstaafu wa Kenya, Mwaki Kibaki kisha saa 3:48 aliingia Uhuru Kenyatta na Rais Uganda, Yoweri Museven.

Baada ya viongozi hao wa kimataifa kuingia, Rais Jakaya Kikwete aliwasili saa 4:20 asubuhi akiwa kwenye gari maalum la wazi na kupokelewa na vifijo na nderemo na wananchi waliokuwa uwanjani hapo.

Rais Kikwete akiwa kwenye msafara uliokuwa na magari matano na pikipiki 24 alizunguka uwanja huku halaiki ya watu ikimpokea kwa kunyoosha kofia na bendera ya taifa juu.

Baadaye, alipanda kwenye jukwaa dogo ambapo mizinga 21 ilipigwa ikiwa ni heshima kwa Rais na kufuatiwa na wimbo wa taifa.

Alikagua gwaride na baadaye maonyesho ya kijeshi yalianza na kutoa nafasi kwa Rais Kikwete na viongozi wengine kushuhudia mazoezi ya askari waendao kwa miguu, anga na majini.

Wanajeshi hao walionyesha zana mbalimbali za kivita zitumiwazo na askari waendao kwa miguu ambapo walipitisha magari mbele ya Rais.

Vilevile, askari watano wa miamvuli walionyesha umahiri wao wa kuruka (Troop Commander) kutoka ndani ya ndege ya kivita kisha kuelea angani umbali wa futi 4,500 kutoka usawa wa bahari na baadaye kutua ardhini.

Kikosi hicho kiliongozwa na Luteni Joseph Kabipe na kuwa kivutuo kikubwa na kusababisha Rais kukiita mbele na kukipongeza kwa kuwapa mikono.

Onyesho lingine lililovutia watu ni la makamandoo wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) linaloongozwa na Luteni Utawangu  ambao walionyesha umahiri wa kupambana na adui kwa kutumia mikono.

Pia jeshi la Magereza lilionyesha mbinu mbalimbali za kukabiliana na uhalifu magerezani  huku jeshi la polisi vikosi vya mbwa na farasi vikionyesha jinsi ya kumkamata mtuhumiwa. 

Sherehe hizo zilibeba kauli mbiu isemayo, Utanzania wetu, ni Muungano wetu, tuulinde, tuuimarishe na kuudumisha.

WAZIMIA
Watu zaidi ya 70  wakiwemo watoto chini ya umri wa miaka 15 walidondoka kutokana na mshituko uliosababishwa na milio ya mizinga iliyolipuliwa viwanjani hapo.

Pia miongoni mwao walidondoka kutokana na njaa, kusimama muda mrefu  na wengine magonjwa.

Msimamizi wa huduma ya kwanza, Dk. Laurence Chipata kutoka Hospitali ya Temeke, alisema kuwa kati ya watu hao  watatu walipelekwa hopitali kwa matibabu zaidi.
Alisema wengine walipewa huduma ya kwanza na kuruhusiwa.

KIKWETE
Katika hotuba yake, Kikwete aliwaeleza nchi jirani  waishi kwa umoja, undugu na kwa upendo.
 
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

Friday, March 28, 2014

Bunge machafuko

  Ni matumizi ya kura zote, wazi na siri
  Mwigulu achafua hali ya hewa
  Ezekiel Wenje awavuruga Mawaziri,Wajumbe
 
Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuani na haki za Bunge Maalum la Katiba, Pandu ZAmeir Kificho (Kushoto), akiwasilisha mapendekezo ya kamati kuhusu butaratibu wa upigaji kura bungeni mjini Dodoma jana,kulia Mjumbe John Mnyika akichangia pia.(Picha na Khalfan Said)
Kitendawili cha kura ya wazi au ya siri limeemdelea kuliandama Bunge Maalum la Katiba kwa kuzua mvutano mkali jana jioni baada ya Kamati ya Kanuni na Haki za Bunge kuwasilisha azimio la kupendekeza utaratibu wa kura ya siri na ya wazi kutumika kupitisha vifungu vya Rasimu ya Katiba.
Jana jioni yalizuka malumbano baada ya Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Pandu Ameir Kificho, kuwasilisha mapendekezo ya azimio la utaratibu wa wajumbe kupiga kura kwa kutumia njia mbili za kura ya wazi na siri kwa kadri kila mjumbe atakavyoona inafaa.

Baada ya kamati hiyo kuwasilisha mapendekezo yake, baadhi ya wajumbe walitoa maoni wengine wakipendekeza kutumika kwa kura ya kielektroniki na wengine wakipinga vikali kwa madai kuwa itakuwa na uchakachuaji.

MAKONDA

Paul Makonda alipendekeza kutumika kwa kura ya kielektroniki ambayo itaokoa muda wa upigaji kura na kila mmoja kufanya kwa uhuru zaidi.

Alisema mvutano uko baina ya wajumbe waliowafuasi wa vyama vya siasa huku 201 wakiwa njiapanda.

PAMELA
Mjumbe Pamela Maasai alisema kura ya elektroniki ni rahisi kuchakachuliwa hivyo siyo vyema Bunge hilo kukubali utaratibu huo na badala yake kura ya siri ambayo itatoa uhuru kwa kila mjumbe kufanya kwa uhuru.

NASSARI
Joshua Nassari aliwataka wajumbe kuacha unafiki na kila mmoja auzungumze kama haifahamu kesho, Katiba iwe neema kwa makundi yote kwa miaka ijayo.

“Bunge moja, taifa moja, katiba moja, nchi moja halafu upigaji kura uwe tofauti, wenzetu wanatengeneza ndege zinaruka bila rubani unasema tumebuni kupiga kura kwa kila kundi kupiga watakavyo…wengi wa wabunge wa CCM wanataka serikali tatu, ila wanashindwa kusema, njia pekee ya kuwasaidia ni kura ya siri,” alisema.

Alisema uchaguzi wa viongozi mbalimbali kura ni ya siri, wajumbe wa Bunge hilo nao wameteuliwa na Rais ambaye alijifungia na kuwateua kwa siri,” alisema na kuongeza kuwa siyo ajabu kwa Bunge hilo kupiga kura ya siri.

OLUOCH
Ezekiel Oluoch alisema kura ya siri ndiyo itasaidia kuiwafanya watu kuwa huru kwa kuwa ndani ya katiba hiyo kuna masuala ya kidini yanayopaswa kuamuliwa kwa usiri.

Alisema kura ya siri inatumika kuamua mambo yenye imani na utata mkubwa kwa kuwa inamsaidia mtu kuwa huru katika kuamua.

LAIZER
Mjumbe Michael Laizer alisema Kamati hiyo imepeleka pendekezo la kutoa suluhisho la utaratibu wa upigaji kura na kama haukubaliki ni wakati wa Mwenyekiti kuwuandikia Rais avunje Bunge ili wajumbe watawanyike na kuondoka Dodoma.

MBOWE

Freeman Mbowe, alisema ni lazima wafike hatua wafanye uamuzi kuliko kuendelea kujadili huku akisema Machi 11, mwaka huu walipitisha kanuni bila kifungu cha 37 na 38 vinavyozungumzia utaratibu wa kura ya wazi na siri.

Alisema utaalamu wa kurushiana maneno na vijembe hausaidii lolote na kwamba ni dhahiri kuwa kwa mazingira ya jana hakuna utaalamu wa kufikia mwafaha kwenye ukumbi kwa kila mmoja kuzungumza kwa kadri utaalamu wake unavyomruhusu.

“Pamoja na utaalamu wetu wa kufanya maamuzi hatuwezi kuliamua suala hili, itakuwa ni aibu tutajikuta kwenye mazingira ya kulazimisha na kuvunja Bunge, hakuna atakayetakoka mshindi si aliyesababisha na ambaye hakusababishiwa,” alisema

Alishauri viongozi wenye busara kukutana na kuzungumza na kuja na uamuzi sahihi kwa kuwa jambo la Katiba ni jambo la maridhiano, hivyo ni lazima kuwe na makubaliano ya kusonga mbele.

MWANGUNGA
Shamsha Mwangunga, alisema wanaotaka kura ya siri ni wanafiki, hawajiamini na wawajui walifanyalo na kwamba ni vyema likafanyika kwa uwazi.

“Tunashindwa kupiga hatua ya mbele kwa kuvutana, hivyo ni vyema kukubali ushauri wa kamati wa kila mmoja kupiga kura anayoona inafaa,” alisema.

RAZA
Mohamed Raza, alisema kura ya wazi ndiyo inayofaa na kwamba kuendelea kulumbana ni kutumia vibaya fedha za Watanzania.

MAKAIDI
Dk. Emmanuel Makaidi alisema kura ya siri itatoa nafasi kwa kila mjumbe kuonyeshana dhamira yake pasipo woga.

“Kura ya elektroniki haifai kuamua, tukubali kura ya siri kama ndiyo msingi wa maamuzi yetu,” alisema.

LEMA
Godbless Lema alisema kura ya siri itawaingiza baadhi ya wajumbe kwenye matatizo kwa kuwa kwa sasa kuna matamko mbalimbali yamesambaa kwenye mitanda ya jamii, vitisho vingi, ikiwamo Zanzibar inasema atakayerudi bila Zanzibar huru kichwa chake kitakuwa halali yao.

Alisema Waziri Mkuu ambaye ni mwenyekiti wa kamati ya wabunge wa CCM akiamua kupiga kura ya siria haamini kama yupo anayeweza kwenda kinyume cha kiongozi wake ambaye amepinga kura ya wazi.

BULAYA
Esther Bulaya alisema msimamo wake ni kura ya siri, lakini amefurahia mapendekezo ya kamati ya kila mmoja kupiga kura kwa nutaratibu anaupenda, hivyo ni vyema wajumbe hao wakakubaliana na kamati.

MWIGULU
Mwigulu Nchemba ambaye pia ni Naibu Waziri wa Fedha, alichafua hali ya hewa baada ya kuwatuhumu Freeman Mbowe na Ismail Jussa Ladhu kuwa wanataka kura ya siri kwa kuwa wanalengo la kuingiza ushoga.

Baada ya kauli ya Nchemba, Profesa Ibrahim Lipumba aliomba mwongozo wa Makamu Mwenyekiti, Samia Suluhu Hassan, akisema Bunge linaangaliwa na watu wa rika tofauti wakiwamo watoto na kwamba Nchemba ametumia lugha isiyo na staha.

Samia alimtaka Nchemba kufuta kauli yake na kuwaomba radhi Mbowe na Jussa, lakini aliendelea kutetea hoja yake akidai kuwa baadhi ya vyama (bila kuvitaja) vinafadhiliwa na nchi zinazokubali ushoga na kwamba ataondoa majina ya Mbowe na Jussa, lakini neno ushoga litabaki pale pale.

Kufuatia kauli za Nchemba, wajumbe waliendelea kupiga kelele na kutaka afute kauli na kuomba radhi, huku Samia akitumia dakika kadhaa kuwatuliza wajumbe na kumtaka Nchemba kufuta kauli na kuomba radhi.

Hata hivyo, baadaye Nchemba alifuta kauli hiyo na kuwaomba radhi Mbowe na Jussa.

MAPENDEKEZO YA KIFICHO

Akiwasilisha Azimio la kufanya marekebisho ya Kanuni za Bunge la Maalum jana, Kificho alisema kuwa marekebisho yanayofanywa ni kanuni za Bunge Maalumu kwenye kanuni ya 37 kwa kuongeza mwishoni mwa fasiri ya (3) maneno “ya siri kwa mjumbe anayetaka kupiga kura ya siri au kura ya wazi kwa mjumbe anayetaka kupiga kura ya wazi kwa kuzingatia utaratibu ulioanishwa katika kanuni ya 38.

WENJE AWASHA MOTO
Kauli ya Ezekiel Wenje kuwa baadhi ya mawaziri wamewahonga baadhi ya wabunge wa makundi ya wabunge 201 ilisababisha vurugu kubwa kwa mawaziri tajwa kutaka waombwe radhi, akiwamo, Profesa Jumanne Maghembe (Maji), Dk. Shukuru Kawambwa (Elimu na Mafunzo ya Ufundi).

Mbali na mawaziri hao pia wajumbe kutoka kundi hilo walitaka kuombwa radhi.

Awali Makamu Mwenyekiti aliyekuwa anaongoza kikao, Samia Suluhu Hassan,  alimtaka Wenje kuomba radhi, lakini alisema mawaziri hao wamethibitisha wenyewe kuwaalika watu hao na kuongeza orodha ya mawaziri kuwa ni pamoja na Gaudensia Kabaka (Kazi na Ajira) na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kwamba walihusika kuwakirimu wajumbe hao na kuwapa msimamo wa serikali mbili.

Wakati vurugu za kelele na kurushiana maneno zikielendelea, Mwenyekiti wa Bunge Maalum, Samuel Sitta, alirejea kwenye kiti chake na kumtaka Wenje amjibu kama kweli haoni kuwa kauli yake imewaudhi wajumbe wengine.

Wenje alisema kuwa inawezekana kuwa kuna watu wameudhika, lakini kwa kuwa alichosema ni ukweli na kwa kuwa anaomba radhi tu, lakini ukweli anausimamia.

Kwa kauli hiyo, Sitta alisema kwa kuwa Wenje amekataa kuomba radhi, basi suala hilo ameamua kulipeleka kwenye kamati ya Kanuni na Haki za Bunge la Bunge Maalum.

Baada ya uamuzi wa Sitta wajumbe walishangilia na Wenje alionekana alishangilia uamuzi huo.
 
CHANZO: NIPASHE

zitto "Tuache kujadili hotuba za JK na Warioba, tuboreshe Rasimu"

zitto b378f
Wiki ya Machi 18 - 22, 2014, mwenyekiti Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba aliwasilisha Rasimu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye Bunge la Katiba.
Wiki hiyo iliishia siku ya Ijumaa ambayo Rais wa Jamhuri ya Muungano, Jakaya Mrisho Kikwete alitoa hotuba kwa Bunge hilo Maalumu.
Hotuba zote zilipokelewa kwa hisia tofauti kulingana na msimamo wa kila mtu kuhusu hoja inayoonekana ni kubwa kuliko zote katika Mchakato wa Kuandika Katiba Mpya, hususan suala la Muundo wa Muungano.(Hudugu Ng'amilo)
Wale wanaoshabikia muundo wa serikali tatu, walifurahishwa mno na hotuba ya Jaji Warioba na wanaoshabikia muundo wa serikali mbili, walifurahishwa mno na hotuba ya Rais Kikwete. Mimi Sikufurahishwa na hotuba zote mbili kwa sababu zifuatazo;
Hotuba hazikunifurahisha
Moja, hotuba zote mbili zilichukua muda mrefu zaidi kuelezea sura moja tu ya Rasimu ya Katiba nayo ni sura ya Sita inayohusu muundo wa Jamhuri ya Muungano kana kwamba Katiba hii inahusu suala hilo pekee.
Ni dhahiri kwamba suala hili ni kubwa na muhimu, kwani linahusu uhai wa dola yenyewe na siwezi kubeza. Hata hivyo, masuala kama Haki za Raia ni muhimu zaidi kwani hata uwe na muundo wa namna gani wa Muungano au hata Muungano wenyewe kuvunjika, bila ya kuwa na haki za msingi za raia, katiba hiyo itakataliwa na wananchi.
Huu mtindo unaozuka wa kudhani muundo wa Muungano ndio mwarobaini wa matatizo ya ufisadi, matumizi mabaya ya madaraka, ubadhirifu, umasikini, elimu ya hovyo, afya dhaifu, utatufikisha pabaya na hata kurudi tena kuandika katiba kwa lengo la kudai haki hizo. Jaji Warioba na Rais Kikwete wameshindwa kuruka kiunzi hicho na kutambua kuwa Katiba ni zaidi ya Muungano.
Pili, Rais Kikwete na Jaji Warioba wamejenga hoja zao kuhusu miundo ya Muungano wanayopendekeza au kuunga mkono kutokana na misingi ama ya 'malalamiko' au 'hofu'.
Jaji Warioba aliorodhesha malalamiko 11 ya upande wa Zanzibar dhidi ya Muungano na malalamiko kumi ya upande wa Bara. Kimsingi malalamiko yote ya upande wa bara yanazaliwa na vitendo vya upande wa Zanzibar, isipokuwa lalamiko namba 'vii' linalohusu kupotea kwa utambulisho wa Tanganyika katika Muundo wa Muungano.
Jaji Warioba anajenga msingi wa pendekezo la tume yake kutokana na kujibu malalamiko au maarufu kama kero za Muungano na anasema "Muundo wa serikali mbili hauwezi kubaki kwa hali ya sasa. Muungano wa serikali mbili waliotuachia waasisi siyo uliopo sasa... waasisi walituachia Muungano wa nchi moja yenye serikali mbili, na siyo nchi mbili zenye Serikali Mbili". Nukuu hii niliipenda kuliko zote katika Hotuba ya Mzee wangu Warioba.
Rais Kikwete alijenga msingi wa maoni yake kwenye hofu za kuwa na serikali tatu. Hofu hizo ni pamoja na gharama za kuendesha Muungano, kuzuka kwa hisia za utaifa wa Utanganyika na Uzanzibari, uwezekano wa Muungano kuvunjika kwa kushindwa kuhudumia majeshi na hata Jeshi kuchukua nchi ikibidi na kutupilia mbali katiba na Serikali ya Muungano kutokuwa na Rasilimali zake.
Rais alisema 'Serikali ya Muungano ni egemezi na tegemezi' nukuu ambayo niliipenda kuliko zote katika Hotuba ya mzee wangu Kikwete.
Lakini Rais hakuniridhisha kabisa namna ya kumaliza kero za Muungano kwa muundo wa sasa kwani umeshindwa kuzimaliza kwa takribani miaka 50 tangu Muungano uundwe.
Haiwezekani muundo uliozalisha kero lukuki ndio utarajiwe kuzimaliza kero hizo. Kwa vyovyote vile ni lazima kuwa na muundo mpya, lakini kiukweli ni lazima muundo huo mpya ujibu hofu alizoeleza Rais maana ni hofu za kweli.
Naye Jaji Warioba hakuniridhisha na namna suala la Uraia litakavyotatuliwa kwani kutoa jibu la kubakia na 'kukubali' nchi mbili halafu uraia mmoja kunatia shaka kubwa. Kama tunataka kuwa na Uraia mmoja ni lazima tuwe nchi moja, hatuwezi kuwa na nchi mbili uraia mmoja.
Pia vyanzo vya mapato ya Muungano ni vidogo mno kuendesha dola. Hivyo rasimu iliyopo ina mapungufu makubwa japo imetoa mapendekezo yatakayomaliza malalamiko.
Kazi ya Bunge sasa ni kuboresha rasimu ili kumaliza kero za Muungano na kuziondoa za hofu za muundo mpya.
Kama kweli tunataka kusikia Watanzania wanataka nini kwenye muundo wa Muungano, tusimamishe Bunge na twende tukawaulize kwa kura ya maoni.
Mwandishi wa makala haya ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini

CHANZO MWANANCHI.

Siri ya CCM kung’ang’ania Serikali mbili kikatiba

katuni 83f0e
Katika maisha ya kawaida, binadamu ana msimamo wake na hata uamuzi asiopenda ubadilike.
Katika medani ya siasa nchini msimamo wa Chama Cha Mapinduzi ( CCM) kuhusu Muungano na muundo unafahamika. Ni muundo wa kutaka Serikali mbili ambao chama hicho unakipigania kwa udi na uvumba.(Hudugu Ng'amilo)
Hata hivyo, msimamo huo ni kinyume na mapendekezo au matakwa ya wengi kama ilivyoainishwa kwenye Rasimu ya Pili ya Katiba iliyoandaliwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Tume hiyo iliyokuwa chini ya Jaji Joseph Warioba ilikusanya maoni ya wananchi na ilipendekeza muundo wa Muungano wa Serikali tatu.
Hivi karibuni akifungua Bunge Maalumu la Katiba, Rais Jakaya Kikwete akaunga mkono msimamo wa chama chake, jambo lililoibua mjadala unaoendelea hadi sasa.
Hoja ya Serikali mbili
Kwanini CCM wanataka Serikali mbili na siyo tatu au moja kama ilivyo maoni ya wananchi walio wengi kwa mujibu wa maelezo ya Tume ya Warioba? Makala haya yanachambua hoja hiyo.
Profesa Bakar Mohammed ni Mhadhiri Mwandamizi na Mkuu wa Idara ya Siasa na Utawala ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, anayesema msimamo wa CCM wa kudai Serikali mbili unatokana na hofu ya uhafidhina wa kuogopa mabadiliko.
Anasema viongozi wengi wa CCM wanasumbuliwa na hofu na woga wa mabadiliko na kwamba wanakuwa wagumu kuyakubali yanapotaka kutokea.
"Kama mtu unaangalia madaraka zaidi, lazima kunakuwa na woga, na hii ni hulka ya binadamu kuwa na woga wa kuacha kile ulichokizoea... Lakini ukiangalia masilahi ya nchi na kuacha yale yanayokusukuma kusingekuwa na wasiwasi huu unaoonekana sasa," anasema.
Anasema CCM inachofanya ni kuhakikisha haking'oki madarakani, huku viongozi wake wakiamini kuwa wana sifa za kuongoza na siyo wengineo.
Profesa Bakari anailinganisha hofu ya sasa ya CCM na ile waliyokuwa nayo viongozi wa chama hicho miaka ya 1990 zilipoanza vuguvugu za mabadiliko ya siasa za vyama vingi. Anasema CCM kiliendesha propaganda kuwa mfumo wa vyama vingi haukuwa na tija na ungeleta vita.0
inShare
Hofu hiyo anasema ndiyo inayokifanya chama hicho kikongwe kuhofia kung'olewa madarakani.
"Woga huo bado upo, wanaogopa pengine mfumo ukiwa wa Serikali tatu uwezekano wa wao kubaki madarakani utakuwa mdogo," anafafanua.
Anaongeza kusema kuwa hofu ya CCM siyo kwa ajili ya masilahi ya nchi, badala yake inaonekana chama kinaangalia masilahi yake.
Ingekuwa vyema anasema kwa CCM kueleza madhara yanayoweza kulikumba taifa ikiwa muundo wa Serikali tatu utapita.
"Wanatoa hoja kuwa mfumo wa Serikali tatu unaweza kusambaratisha nchi, lakini hakuna uhakika kama mfumo huu uliopo nchi hauwezi kusambaratika," anasema.
Hofu ya kuyumba na kuanguka
Mhadhiri mwingine wa chuo hicho, Dk. Benson Bana anasema siri ya CCM kung'ang'ania Serikali mbili inatokana na hofu ya kuyumba na kuanguka.
Anasema CCM kimekuwa madarakani na mfumo huo kwa miaka 50 na kwamba hofu yao ni kuwa ukiondoa Serikali mbili kinaweza kuyumba na kuachia madaraka.

Anasema misingi ya wanasiasa ni madaraka, na kwamba ukishayapata, huwezi kuyaachia kirahisi.
"Misingi ya wanasiasa ni madaraka... Kuyalinda, kuyahifadhi na kuyatumia madaraka yale kwa namna yoyote...Huwezi kuyaachia madaraka kirahisi. Utafanya ujanja, utatumia mbinu chafu ili tu kuhakikisha unabaki madarakani, na hiki ndicho wanachofanya CCM," anasema.

Dk. Bana anasema CCM kingeeleweka na kingekuwa na mwonekano mzuri zaidi endapo wangepigania kuwapo kwa Serikali moja.

"Wangekuwa wanataka muungano imara, endelevu na uliokomaa wangeelekeza katika Serikali moja...Lakini hawataki kwa sababu wanajua moja inaweza ikawanyima uongozi," anasema.Dk. Bana anasema ni vyema wananchi wakaelimishwa huu muungano una faida gani na wanafunzi shuleni katika elimu ya uraia waelezwe faida zake.

"Ingekuwa wazi tungejua nani anafaidika na nini, mikopo misaada, nani anachangia nini...Je zile sababu za waasisi za kuungana bado zipo sasa miaka 50 ya Muungano, ule woga kuwa Zanzibar itamezwa bado upo leo?" Anahoji.

Anaongeza kuwa ni vyema kwa watawala kutazama mazingira ya sasa ya siasa zetu kwa kile anachoeleza kuwa hata Katiba ikipita ikakubali kuwapo wa Serikali mbili, bado wananchi watahoji mantiki ya muundo huo.

Msomi mwingine wa siasa, Dk. Alexander Makuliko anasema hofu ya CCM ni kuwa ndio iliyouasisi Muungano wa Serikali mbili, hivyo isingependa hali hiyo ibadilike.

Anaendelea kusema kuwa CCM imezoea mfumo huu na kuwa ikiukosa itaathirika, kwakuwa ni sera yake na imekuwa ikiitekeleza, lakini msimamo wa wananchi ndiyo kitu cha msingi kuzingatiwa. Hoja zijengwe na zisikilizwe, ubabe hautakiwi, busara inahitajika zaidi.
Anasema pamoja na suala la Serikali mbili kuwa ni pimajoto ya uhai wa CCM, hata hivyo hoja zinazotolewa katika kutetea msimamo wao ni nzuri tu na zinazoeleweka vyema.

"Sioni kama wanang'ang'ania, lakini ukweli ni kuwa kila chama kina sera yake, na CCM kimeweka sera yake katika suala la Muungano wao wanasema ni Serikali mbili, na siyo tatu...kwamba tatu zitaongeza gharama na mengineyo, ni sababu za msingi kabisa," anasema.

Anaongeza kuwa hoja zinazotolewa na chama tawala ni kubwa na siyo za kupuuzwa, lakini vilevile kero zinazotajwa kuhusu mfumo wa Muungano uliopo nazo zipo na zinaweza kutatuliwa katika mfumo uliopo.

"Unajua hivi vyama kila kimoja kinataka kuvutia kwake, hata bila rasimu ya Warioba...Ninashauri walete hoja, kisha watu wazipime hizo hoja, kwanini serikali mbili, na wale wa tatu tayari wameleta hoja na ushahidi, watu waachwe wapime," anasema na kuongeza:

''Jambo la msingi kuzingatiwa ni kuwa mawazo ya wananchi wengi yataonekana wakati wa kura za maoni. Angalizo ni kuhakikisha kuwa kura hiyo isije ikachakachuliwa.''

CHANZO MWANANCHI