Thursday, July 11, 2013

Aliyeruhusu masanduku ya Agnes na Melisa yapite na dawa za kulevya JNIA... (?)

Polisi imekiri kuwa wasichana wawili raia wa Tanzania waliokamatwa nchini Afrika Kusini wakiwa na dawa za kulevya zenye thamani ya Sh. bilioni 6.8, walipitia katika Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu Julius Nyerere, jijini Dar es Salaam.

Wasichana hao walisafiri kwa ndege ya Shirika la Ndege la South African Airways linalomilikiwa na serikali ya Afrika Kusini.

Kamanda wa Polisi Kitengo cha Kuzuia na Kupambana na Dawa za Kulevya, Geofrey Nzoa, alisema hayo jana wakati akizungumza katika mahojiano na NIPASHE iliyotaka kujua kama wasichana hao walipitia uwanja gani na kama walikaguliwa na maofisa wa uwanja huo.

“Kila mtu anapopita uwanja wa ndege anakaguliwa na kama ana kitu ambacho ni kibaya ndipo anakamatwa, hawa wasichana walikaguliwa maana huwezi kupita uwanja wa ndege bila kukaguliwa,” alisema Kamanda Nzoa.

Kamanda Nzoa alisema si jukumu la Jeshi la Polisi kufanya ukaguzi kwenye viwanja vya ndege, lakini ni 
jambo la kawaida mtu kukamatwa nchi nyingine na dawa za kulevya wakati katika nchi aliyoanzia safari hajakamatwa kwani inategemea utalaamu wa watu wenyewe wanaokagua.

Alisema kinachotakiwa watu wa uwanja wa ndege ni lazima wawe na mtu au wakaguzi ambaye ni mtaalamu sana wa kutambua dawa za kulevya kwa kuwa ziko za aina nyingi na mbinu nyingi zinatumika kuzisafirisha.
Aidha, alisema dawa za kulevya ni nyingi na siyo cocaine tu ambayo imezoeleka mara kwa mara.

“Utakumbuka Juni 23 mwaka 2010 nilikamata mabalozi wawili, hawa watu walitoka Brazil wakaenda Afrika Kusini, lakini tukawakamatia hapa Tanzania,” alisema Nzoa.

Aliongeza kuwa hivi sasa wasichana  hao wamekwisha kufunguliwa mashtaka nchini Afrika Kusini.

Kamanda Nzoa alisema uchunguzi unaendelea kumbaini mmiliki wa dawa hizo na kuna dalili za kuwabaini wahusika hao.

Dawa hizo zilisafirishwa kama mizigo mingine inayokaa sehemu za mizigo ndani  ya ndege kwani uzoefu unaonyesha kwamba kwa namna yoyote ile abiria hawezi kuruhusiwa kwenda  kukaa na mzigo wake ndani ya ndege unaofikia kilo 150.

Uzoefu unaonyesha kwamba kwa kawaida ndege kulingana na ukubwa wake zimekuwa zikiruhusu abiria kupanda na kukaa na mizigo yao ya mkononi isiyo na uzito mkubwa.

Baadhi ya ndege zinaruhusu abiria kupanda ndani ya ndege wakiwa na mizigo yao ya mkononi isiyozidi uzito wa kilo kumi wakati mzigo unaokaa kwenye mizigo chini baadhi ya mashirika ya ndege huruhusu uzito wa kuanzia kilo 20 hadi 40.

Katika hali ya kawaida, hata kama wasichana hao wangeamua kugawana dawa hizo kwa usawa, kila mmoja angebeba kilo 75, kiasi ambacho hata hivyo abiria haruhusiwi kupanda nacho kama mzigo wa mkononi, wala mzigo ambao haulipiwi.

Kwa hali hiyo, mizigo hiyo ililipiwa gharama za ziada za usafirishaji kwa kuwa hakuna shirika la ndege lenye unafuu wa mizigo ya bure kwa abiria wake kwa uzito wa kilo 75.

Jitihada zinaendelea kumtafuta Mkurugenzi Mkuu wa Mamlaka ya Viwanja vya Ndege Nchini (TAA), kujua ilikuwa je watumishi waliokuwa zamu siku ambayo mzigo huo ulisafirishwa kuelekea nchini Afrika Kusini hawakutambua dawa hizo.

--- Imeandiwa na THOBIAS MWANAKATWE via gazeti la NIPASHE

No comments:

Post a Comment