Friday, March 28, 2014

Bunge machafuko

  Ni matumizi ya kura zote, wazi na siri
  Mwigulu achafua hali ya hewa
  Ezekiel Wenje awavuruga Mawaziri,Wajumbe
 
Mwenyekiti wa Kamati ya Kanuani na haki za Bunge Maalum la Katiba, Pandu ZAmeir Kificho (Kushoto), akiwasilisha mapendekezo ya kamati kuhusu butaratibu wa upigaji kura bungeni mjini Dodoma jana,kulia Mjumbe John Mnyika akichangia pia.(Picha na Khalfan Said)
Kitendawili cha kura ya wazi au ya siri limeemdelea kuliandama Bunge Maalum la Katiba kwa kuzua mvutano mkali jana jioni baada ya Kamati ya Kanuni na Haki za Bunge kuwasilisha azimio la kupendekeza utaratibu wa kura ya siri na ya wazi kutumika kupitisha vifungu vya Rasimu ya Katiba.
Jana jioni yalizuka malumbano baada ya Mwenyekiti wa Kamati hiyo, Pandu Ameir Kificho, kuwasilisha mapendekezo ya azimio la utaratibu wa wajumbe kupiga kura kwa kutumia njia mbili za kura ya wazi na siri kwa kadri kila mjumbe atakavyoona inafaa.

Baada ya kamati hiyo kuwasilisha mapendekezo yake, baadhi ya wajumbe walitoa maoni wengine wakipendekeza kutumika kwa kura ya kielektroniki na wengine wakipinga vikali kwa madai kuwa itakuwa na uchakachuaji.

MAKONDA

Paul Makonda alipendekeza kutumika kwa kura ya kielektroniki ambayo itaokoa muda wa upigaji kura na kila mmoja kufanya kwa uhuru zaidi.

Alisema mvutano uko baina ya wajumbe waliowafuasi wa vyama vya siasa huku 201 wakiwa njiapanda.

PAMELA
Mjumbe Pamela Maasai alisema kura ya elektroniki ni rahisi kuchakachuliwa hivyo siyo vyema Bunge hilo kukubali utaratibu huo na badala yake kura ya siri ambayo itatoa uhuru kwa kila mjumbe kufanya kwa uhuru.

NASSARI
Joshua Nassari aliwataka wajumbe kuacha unafiki na kila mmoja auzungumze kama haifahamu kesho, Katiba iwe neema kwa makundi yote kwa miaka ijayo.

“Bunge moja, taifa moja, katiba moja, nchi moja halafu upigaji kura uwe tofauti, wenzetu wanatengeneza ndege zinaruka bila rubani unasema tumebuni kupiga kura kwa kila kundi kupiga watakavyo…wengi wa wabunge wa CCM wanataka serikali tatu, ila wanashindwa kusema, njia pekee ya kuwasaidia ni kura ya siri,” alisema.

Alisema uchaguzi wa viongozi mbalimbali kura ni ya siri, wajumbe wa Bunge hilo nao wameteuliwa na Rais ambaye alijifungia na kuwateua kwa siri,” alisema na kuongeza kuwa siyo ajabu kwa Bunge hilo kupiga kura ya siri.

OLUOCH
Ezekiel Oluoch alisema kura ya siri ndiyo itasaidia kuiwafanya watu kuwa huru kwa kuwa ndani ya katiba hiyo kuna masuala ya kidini yanayopaswa kuamuliwa kwa usiri.

Alisema kura ya siri inatumika kuamua mambo yenye imani na utata mkubwa kwa kuwa inamsaidia mtu kuwa huru katika kuamua.

LAIZER
Mjumbe Michael Laizer alisema Kamati hiyo imepeleka pendekezo la kutoa suluhisho la utaratibu wa upigaji kura na kama haukubaliki ni wakati wa Mwenyekiti kuwuandikia Rais avunje Bunge ili wajumbe watawanyike na kuondoka Dodoma.

MBOWE

Freeman Mbowe, alisema ni lazima wafike hatua wafanye uamuzi kuliko kuendelea kujadili huku akisema Machi 11, mwaka huu walipitisha kanuni bila kifungu cha 37 na 38 vinavyozungumzia utaratibu wa kura ya wazi na siri.

Alisema utaalamu wa kurushiana maneno na vijembe hausaidii lolote na kwamba ni dhahiri kuwa kwa mazingira ya jana hakuna utaalamu wa kufikia mwafaha kwenye ukumbi kwa kila mmoja kuzungumza kwa kadri utaalamu wake unavyomruhusu.

“Pamoja na utaalamu wetu wa kufanya maamuzi hatuwezi kuliamua suala hili, itakuwa ni aibu tutajikuta kwenye mazingira ya kulazimisha na kuvunja Bunge, hakuna atakayetakoka mshindi si aliyesababisha na ambaye hakusababishiwa,” alisema

Alishauri viongozi wenye busara kukutana na kuzungumza na kuja na uamuzi sahihi kwa kuwa jambo la Katiba ni jambo la maridhiano, hivyo ni lazima kuwe na makubaliano ya kusonga mbele.

MWANGUNGA
Shamsha Mwangunga, alisema wanaotaka kura ya siri ni wanafiki, hawajiamini na wawajui walifanyalo na kwamba ni vyema likafanyika kwa uwazi.

“Tunashindwa kupiga hatua ya mbele kwa kuvutana, hivyo ni vyema kukubali ushauri wa kamati wa kila mmoja kupiga kura anayoona inafaa,” alisema.

RAZA
Mohamed Raza, alisema kura ya wazi ndiyo inayofaa na kwamba kuendelea kulumbana ni kutumia vibaya fedha za Watanzania.

MAKAIDI
Dk. Emmanuel Makaidi alisema kura ya siri itatoa nafasi kwa kila mjumbe kuonyeshana dhamira yake pasipo woga.

“Kura ya elektroniki haifai kuamua, tukubali kura ya siri kama ndiyo msingi wa maamuzi yetu,” alisema.

LEMA
Godbless Lema alisema kura ya siri itawaingiza baadhi ya wajumbe kwenye matatizo kwa kuwa kwa sasa kuna matamko mbalimbali yamesambaa kwenye mitanda ya jamii, vitisho vingi, ikiwamo Zanzibar inasema atakayerudi bila Zanzibar huru kichwa chake kitakuwa halali yao.

Alisema Waziri Mkuu ambaye ni mwenyekiti wa kamati ya wabunge wa CCM akiamua kupiga kura ya siria haamini kama yupo anayeweza kwenda kinyume cha kiongozi wake ambaye amepinga kura ya wazi.

BULAYA
Esther Bulaya alisema msimamo wake ni kura ya siri, lakini amefurahia mapendekezo ya kamati ya kila mmoja kupiga kura kwa nutaratibu anaupenda, hivyo ni vyema wajumbe hao wakakubaliana na kamati.

MWIGULU
Mwigulu Nchemba ambaye pia ni Naibu Waziri wa Fedha, alichafua hali ya hewa baada ya kuwatuhumu Freeman Mbowe na Ismail Jussa Ladhu kuwa wanataka kura ya siri kwa kuwa wanalengo la kuingiza ushoga.

Baada ya kauli ya Nchemba, Profesa Ibrahim Lipumba aliomba mwongozo wa Makamu Mwenyekiti, Samia Suluhu Hassan, akisema Bunge linaangaliwa na watu wa rika tofauti wakiwamo watoto na kwamba Nchemba ametumia lugha isiyo na staha.

Samia alimtaka Nchemba kufuta kauli yake na kuwaomba radhi Mbowe na Jussa, lakini aliendelea kutetea hoja yake akidai kuwa baadhi ya vyama (bila kuvitaja) vinafadhiliwa na nchi zinazokubali ushoga na kwamba ataondoa majina ya Mbowe na Jussa, lakini neno ushoga litabaki pale pale.

Kufuatia kauli za Nchemba, wajumbe waliendelea kupiga kelele na kutaka afute kauli na kuomba radhi, huku Samia akitumia dakika kadhaa kuwatuliza wajumbe na kumtaka Nchemba kufuta kauli na kuomba radhi.

Hata hivyo, baadaye Nchemba alifuta kauli hiyo na kuwaomba radhi Mbowe na Jussa.

MAPENDEKEZO YA KIFICHO

Akiwasilisha Azimio la kufanya marekebisho ya Kanuni za Bunge la Maalum jana, Kificho alisema kuwa marekebisho yanayofanywa ni kanuni za Bunge Maalumu kwenye kanuni ya 37 kwa kuongeza mwishoni mwa fasiri ya (3) maneno “ya siri kwa mjumbe anayetaka kupiga kura ya siri au kura ya wazi kwa mjumbe anayetaka kupiga kura ya wazi kwa kuzingatia utaratibu ulioanishwa katika kanuni ya 38.

WENJE AWASHA MOTO
Kauli ya Ezekiel Wenje kuwa baadhi ya mawaziri wamewahonga baadhi ya wabunge wa makundi ya wabunge 201 ilisababisha vurugu kubwa kwa mawaziri tajwa kutaka waombwe radhi, akiwamo, Profesa Jumanne Maghembe (Maji), Dk. Shukuru Kawambwa (Elimu na Mafunzo ya Ufundi).

Mbali na mawaziri hao pia wajumbe kutoka kundi hilo walitaka kuombwa radhi.

Awali Makamu Mwenyekiti aliyekuwa anaongoza kikao, Samia Suluhu Hassan,  alimtaka Wenje kuomba radhi, lakini alisema mawaziri hao wamethibitisha wenyewe kuwaalika watu hao na kuongeza orodha ya mawaziri kuwa ni pamoja na Gaudensia Kabaka (Kazi na Ajira) na Waziri Mkuu, Mizengo Pinda, kwamba walihusika kuwakirimu wajumbe hao na kuwapa msimamo wa serikali mbili.

Wakati vurugu za kelele na kurushiana maneno zikielendelea, Mwenyekiti wa Bunge Maalum, Samuel Sitta, alirejea kwenye kiti chake na kumtaka Wenje amjibu kama kweli haoni kuwa kauli yake imewaudhi wajumbe wengine.

Wenje alisema kuwa inawezekana kuwa kuna watu wameudhika, lakini kwa kuwa alichosema ni ukweli na kwa kuwa anaomba radhi tu, lakini ukweli anausimamia.

Kwa kauli hiyo, Sitta alisema kwa kuwa Wenje amekataa kuomba radhi, basi suala hilo ameamua kulipeleka kwenye kamati ya Kanuni na Haki za Bunge la Bunge Maalum.

Baada ya uamuzi wa Sitta wajumbe walishangilia na Wenje alionekana alishangilia uamuzi huo.
 
CHANZO: NIPASHE

zitto "Tuache kujadili hotuba za JK na Warioba, tuboreshe Rasimu"

zitto b378f
Wiki ya Machi 18 - 22, 2014, mwenyekiti Tume ya Mabadiliko ya Katiba, Jaji Joseph Warioba aliwasilisha Rasimu ya Katiba ya Jamhuri ya Muungano wa Tanzania kwenye Bunge la Katiba.
Wiki hiyo iliishia siku ya Ijumaa ambayo Rais wa Jamhuri ya Muungano, Jakaya Mrisho Kikwete alitoa hotuba kwa Bunge hilo Maalumu.
Hotuba zote zilipokelewa kwa hisia tofauti kulingana na msimamo wa kila mtu kuhusu hoja inayoonekana ni kubwa kuliko zote katika Mchakato wa Kuandika Katiba Mpya, hususan suala la Muundo wa Muungano.(Hudugu Ng'amilo)
Wale wanaoshabikia muundo wa serikali tatu, walifurahishwa mno na hotuba ya Jaji Warioba na wanaoshabikia muundo wa serikali mbili, walifurahishwa mno na hotuba ya Rais Kikwete. Mimi Sikufurahishwa na hotuba zote mbili kwa sababu zifuatazo;
Hotuba hazikunifurahisha
Moja, hotuba zote mbili zilichukua muda mrefu zaidi kuelezea sura moja tu ya Rasimu ya Katiba nayo ni sura ya Sita inayohusu muundo wa Jamhuri ya Muungano kana kwamba Katiba hii inahusu suala hilo pekee.
Ni dhahiri kwamba suala hili ni kubwa na muhimu, kwani linahusu uhai wa dola yenyewe na siwezi kubeza. Hata hivyo, masuala kama Haki za Raia ni muhimu zaidi kwani hata uwe na muundo wa namna gani wa Muungano au hata Muungano wenyewe kuvunjika, bila ya kuwa na haki za msingi za raia, katiba hiyo itakataliwa na wananchi.
Huu mtindo unaozuka wa kudhani muundo wa Muungano ndio mwarobaini wa matatizo ya ufisadi, matumizi mabaya ya madaraka, ubadhirifu, umasikini, elimu ya hovyo, afya dhaifu, utatufikisha pabaya na hata kurudi tena kuandika katiba kwa lengo la kudai haki hizo. Jaji Warioba na Rais Kikwete wameshindwa kuruka kiunzi hicho na kutambua kuwa Katiba ni zaidi ya Muungano.
Pili, Rais Kikwete na Jaji Warioba wamejenga hoja zao kuhusu miundo ya Muungano wanayopendekeza au kuunga mkono kutokana na misingi ama ya 'malalamiko' au 'hofu'.
Jaji Warioba aliorodhesha malalamiko 11 ya upande wa Zanzibar dhidi ya Muungano na malalamiko kumi ya upande wa Bara. Kimsingi malalamiko yote ya upande wa bara yanazaliwa na vitendo vya upande wa Zanzibar, isipokuwa lalamiko namba 'vii' linalohusu kupotea kwa utambulisho wa Tanganyika katika Muundo wa Muungano.
Jaji Warioba anajenga msingi wa pendekezo la tume yake kutokana na kujibu malalamiko au maarufu kama kero za Muungano na anasema "Muundo wa serikali mbili hauwezi kubaki kwa hali ya sasa. Muungano wa serikali mbili waliotuachia waasisi siyo uliopo sasa... waasisi walituachia Muungano wa nchi moja yenye serikali mbili, na siyo nchi mbili zenye Serikali Mbili". Nukuu hii niliipenda kuliko zote katika Hotuba ya Mzee wangu Warioba.
Rais Kikwete alijenga msingi wa maoni yake kwenye hofu za kuwa na serikali tatu. Hofu hizo ni pamoja na gharama za kuendesha Muungano, kuzuka kwa hisia za utaifa wa Utanganyika na Uzanzibari, uwezekano wa Muungano kuvunjika kwa kushindwa kuhudumia majeshi na hata Jeshi kuchukua nchi ikibidi na kutupilia mbali katiba na Serikali ya Muungano kutokuwa na Rasilimali zake.
Rais alisema 'Serikali ya Muungano ni egemezi na tegemezi' nukuu ambayo niliipenda kuliko zote katika Hotuba ya mzee wangu Kikwete.
Lakini Rais hakuniridhisha kabisa namna ya kumaliza kero za Muungano kwa muundo wa sasa kwani umeshindwa kuzimaliza kwa takribani miaka 50 tangu Muungano uundwe.
Haiwezekani muundo uliozalisha kero lukuki ndio utarajiwe kuzimaliza kero hizo. Kwa vyovyote vile ni lazima kuwa na muundo mpya, lakini kiukweli ni lazima muundo huo mpya ujibu hofu alizoeleza Rais maana ni hofu za kweli.
Naye Jaji Warioba hakuniridhisha na namna suala la Uraia litakavyotatuliwa kwani kutoa jibu la kubakia na 'kukubali' nchi mbili halafu uraia mmoja kunatia shaka kubwa. Kama tunataka kuwa na Uraia mmoja ni lazima tuwe nchi moja, hatuwezi kuwa na nchi mbili uraia mmoja.
Pia vyanzo vya mapato ya Muungano ni vidogo mno kuendesha dola. Hivyo rasimu iliyopo ina mapungufu makubwa japo imetoa mapendekezo yatakayomaliza malalamiko.
Kazi ya Bunge sasa ni kuboresha rasimu ili kumaliza kero za Muungano na kuziondoa za hofu za muundo mpya.
Kama kweli tunataka kusikia Watanzania wanataka nini kwenye muundo wa Muungano, tusimamishe Bunge na twende tukawaulize kwa kura ya maoni.
Mwandishi wa makala haya ni Mbunge wa Kigoma Kaskazini

CHANZO MWANANCHI.

Siri ya CCM kung’ang’ania Serikali mbili kikatiba

katuni 83f0e
Katika maisha ya kawaida, binadamu ana msimamo wake na hata uamuzi asiopenda ubadilike.
Katika medani ya siasa nchini msimamo wa Chama Cha Mapinduzi ( CCM) kuhusu Muungano na muundo unafahamika. Ni muundo wa kutaka Serikali mbili ambao chama hicho unakipigania kwa udi na uvumba.(Hudugu Ng'amilo)
Hata hivyo, msimamo huo ni kinyume na mapendekezo au matakwa ya wengi kama ilivyoainishwa kwenye Rasimu ya Pili ya Katiba iliyoandaliwa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Tume hiyo iliyokuwa chini ya Jaji Joseph Warioba ilikusanya maoni ya wananchi na ilipendekeza muundo wa Muungano wa Serikali tatu.
Hivi karibuni akifungua Bunge Maalumu la Katiba, Rais Jakaya Kikwete akaunga mkono msimamo wa chama chake, jambo lililoibua mjadala unaoendelea hadi sasa.
Hoja ya Serikali mbili
Kwanini CCM wanataka Serikali mbili na siyo tatu au moja kama ilivyo maoni ya wananchi walio wengi kwa mujibu wa maelezo ya Tume ya Warioba? Makala haya yanachambua hoja hiyo.
Profesa Bakar Mohammed ni Mhadhiri Mwandamizi na Mkuu wa Idara ya Siasa na Utawala ya Chuo Kikuu cha Dar es Salaam, anayesema msimamo wa CCM wa kudai Serikali mbili unatokana na hofu ya uhafidhina wa kuogopa mabadiliko.
Anasema viongozi wengi wa CCM wanasumbuliwa na hofu na woga wa mabadiliko na kwamba wanakuwa wagumu kuyakubali yanapotaka kutokea.
"Kama mtu unaangalia madaraka zaidi, lazima kunakuwa na woga, na hii ni hulka ya binadamu kuwa na woga wa kuacha kile ulichokizoea... Lakini ukiangalia masilahi ya nchi na kuacha yale yanayokusukuma kusingekuwa na wasiwasi huu unaoonekana sasa," anasema.
Anasema CCM inachofanya ni kuhakikisha haking'oki madarakani, huku viongozi wake wakiamini kuwa wana sifa za kuongoza na siyo wengineo.
Profesa Bakari anailinganisha hofu ya sasa ya CCM na ile waliyokuwa nayo viongozi wa chama hicho miaka ya 1990 zilipoanza vuguvugu za mabadiliko ya siasa za vyama vingi. Anasema CCM kiliendesha propaganda kuwa mfumo wa vyama vingi haukuwa na tija na ungeleta vita.0
inShare
Hofu hiyo anasema ndiyo inayokifanya chama hicho kikongwe kuhofia kung'olewa madarakani.
"Woga huo bado upo, wanaogopa pengine mfumo ukiwa wa Serikali tatu uwezekano wa wao kubaki madarakani utakuwa mdogo," anafafanua.
Anaongeza kusema kuwa hofu ya CCM siyo kwa ajili ya masilahi ya nchi, badala yake inaonekana chama kinaangalia masilahi yake.
Ingekuwa vyema anasema kwa CCM kueleza madhara yanayoweza kulikumba taifa ikiwa muundo wa Serikali tatu utapita.
"Wanatoa hoja kuwa mfumo wa Serikali tatu unaweza kusambaratisha nchi, lakini hakuna uhakika kama mfumo huu uliopo nchi hauwezi kusambaratika," anasema.
Hofu ya kuyumba na kuanguka
Mhadhiri mwingine wa chuo hicho, Dk. Benson Bana anasema siri ya CCM kung'ang'ania Serikali mbili inatokana na hofu ya kuyumba na kuanguka.
Anasema CCM kimekuwa madarakani na mfumo huo kwa miaka 50 na kwamba hofu yao ni kuwa ukiondoa Serikali mbili kinaweza kuyumba na kuachia madaraka.

Anasema misingi ya wanasiasa ni madaraka, na kwamba ukishayapata, huwezi kuyaachia kirahisi.
"Misingi ya wanasiasa ni madaraka... Kuyalinda, kuyahifadhi na kuyatumia madaraka yale kwa namna yoyote...Huwezi kuyaachia madaraka kirahisi. Utafanya ujanja, utatumia mbinu chafu ili tu kuhakikisha unabaki madarakani, na hiki ndicho wanachofanya CCM," anasema.

Dk. Bana anasema CCM kingeeleweka na kingekuwa na mwonekano mzuri zaidi endapo wangepigania kuwapo kwa Serikali moja.

"Wangekuwa wanataka muungano imara, endelevu na uliokomaa wangeelekeza katika Serikali moja...Lakini hawataki kwa sababu wanajua moja inaweza ikawanyima uongozi," anasema.Dk. Bana anasema ni vyema wananchi wakaelimishwa huu muungano una faida gani na wanafunzi shuleni katika elimu ya uraia waelezwe faida zake.

"Ingekuwa wazi tungejua nani anafaidika na nini, mikopo misaada, nani anachangia nini...Je zile sababu za waasisi za kuungana bado zipo sasa miaka 50 ya Muungano, ule woga kuwa Zanzibar itamezwa bado upo leo?" Anahoji.

Anaongeza kuwa ni vyema kwa watawala kutazama mazingira ya sasa ya siasa zetu kwa kile anachoeleza kuwa hata Katiba ikipita ikakubali kuwapo wa Serikali mbili, bado wananchi watahoji mantiki ya muundo huo.

Msomi mwingine wa siasa, Dk. Alexander Makuliko anasema hofu ya CCM ni kuwa ndio iliyouasisi Muungano wa Serikali mbili, hivyo isingependa hali hiyo ibadilike.

Anaendelea kusema kuwa CCM imezoea mfumo huu na kuwa ikiukosa itaathirika, kwakuwa ni sera yake na imekuwa ikiitekeleza, lakini msimamo wa wananchi ndiyo kitu cha msingi kuzingatiwa. Hoja zijengwe na zisikilizwe, ubabe hautakiwi, busara inahitajika zaidi.
Anasema pamoja na suala la Serikali mbili kuwa ni pimajoto ya uhai wa CCM, hata hivyo hoja zinazotolewa katika kutetea msimamo wao ni nzuri tu na zinazoeleweka vyema.

"Sioni kama wanang'ang'ania, lakini ukweli ni kuwa kila chama kina sera yake, na CCM kimeweka sera yake katika suala la Muungano wao wanasema ni Serikali mbili, na siyo tatu...kwamba tatu zitaongeza gharama na mengineyo, ni sababu za msingi kabisa," anasema.

Anaongeza kuwa hoja zinazotolewa na chama tawala ni kubwa na siyo za kupuuzwa, lakini vilevile kero zinazotajwa kuhusu mfumo wa Muungano uliopo nazo zipo na zinaweza kutatuliwa katika mfumo uliopo.

"Unajua hivi vyama kila kimoja kinataka kuvutia kwake, hata bila rasimu ya Warioba...Ninashauri walete hoja, kisha watu wazipime hizo hoja, kwanini serikali mbili, na wale wa tatu tayari wameleta hoja na ushahidi, watu waachwe wapime," anasema na kuongeza:

''Jambo la msingi kuzingatiwa ni kuwa mawazo ya wananchi wengi yataonekana wakati wa kura za maoni. Angalizo ni kuhakikisha kuwa kura hiyo isije ikachakachuliwa.''

CHANZO MWANANCHI

Seif: Hatuko tayari kujadili serikali mbili

maalim 229b9

Mapendekezo yaliyowasilishwa na Jaji Warioba hayakuwa maoni yake, yale ni maoni ya wananchi, Tanganyika imevaa koti la Muungano, ametoa ushahidi wake ili kujenga mwafaka katika kuendeleza Muungano wenye mfumo wa serikali tatu,"

 Zanzibar. Makamu wa Kwanza wa Serikali ya Mapinduzi Zanzibar, Maalim Seif Sharif Hamad amesema chama chake cha CUF hakiko tayari kujadili mfumo wa Muungano wa serikali mbili kama inavyotetewa na wabunge wa CCM na Rais Jakaya Kikwete.

Amesema tayari amewaandikia barua Rais Kikwete na Rais wa Zanzibar, Dk Ali Mohamed Shein kuwaeleza juu ya msimamo huo.

Maalim Seif alitoa msimamo huo jana kwenye mkutano wa hadhara uliofanyika kwenye viwanja vya Kibandamaiti mjini Unguja.(Hudugu Ng'amilo)

Isitoshe, alisema CUF imebaini kuwa kuna njama za kufuta kipengele katika Katiba ya Zanzibar kinachosema; "Zanzibar ni nchi" na kwamba hiyo ni sawa na kutwanga maji kwenye kinu kwa kuwa Wazanzibari kamwe hawatakubali kufanya hivyo.

Maalim Seif alisema haikuwa mwafaka kwa Rais Kikwete kukosoa mapendekezo ya Rasimu ya Katiba yanayotaka mfumo wa Muungano kuwa wa serikali tatu.

Alisema Jaji Warioba aliweka kando itikadi yake ya CCM katika utendaji wake kwenye Tume ya Mabadiliko ya Katiba na kuja na uamuzi huo kwa vile ndiyo tiba ya kero za Muungano wa Tanganyika na Zanzibar.

"Mapendekezo yaliyowasilishwa na Jaji Warioba hayakuwa maoni yake, yale ni maoni ya wananchi, Tanganyika imevaa koti la Muungano, ametoa ushahidi wake ili kujenga mwafaka katika kuendeleza Muungano wenye mfumo wa serikali tatu," alisema Maalim Seif.

Alisema Muungano wa serikali mbili hauvumiliki na kama kuna watu wanaendelea kuutetea mfumo huo, Zanzibar inaweza kutumia sheria yake ya kura ya maoni kuwauliza wananchi wanaotaka na wasiotaka jambo hilo.

"Nimemwandikia barua Rais Kikwete, nakala nimempelekea Rais wa Zanzibar Dk Ali Mohamed Shein, Tanzania Bara wanataka Zanzibar iondoe kifungu cha Katiba kinachosema Zanzibar ni nchi, jambo hilo halitapita...tutafanya kampeni wananchi walikatae," alieleza Katibu Mkuu huyo wa CUF.

Alisema ni jambo la kusikitisha katika hotuba yake alijisahau kama ni mkuu wa nchi na analihutubia Bunge Maalumu badala yake akaegemea kuwa mwenyekiti wa CCM.

Alisema haikuwa sahihi kutoa vitisho na kutaja ikiwa Serikali ya Muungano chini ya Serikali tatu italegalega, jeshi litachukua madaraka ya nchi.

"Rafiki na ndugu yangu Kikwete, usifikiri huu ni wakati ule wa Julius Nyerere, akisema yeye hakuna wa kumpinga. Mambo yamebadilika, usijifanye ni Nyerere mpya, hakuna atakayekusikiliza na kubabaika," alisisitiza Maalim Seif.Alisema ikiwa viongozi wa Muungano wanajiandaa kutisha watu na kusababisha ghasia katika nchi, mahakama ya kimataifa ya makosa ya jinai ipo na watakaosababisha fujo na umwagaji wa damu watafikishwa mbele ya mikono ya sheria bila ya kujali nyadhifa na madaraka yao.

CHANZO MWANANCHI

Mnara wa Katiba.....ni Kama Mnara wa Babeli.....!






OBAMA AKUTANA NA PAPA FRANCIS- VATICAN

Friday, March 7, 2014

Safari ya kupata Katiba Mpya giza totoro mbele

Mwenyekiti wa muda Bunge la katiba,Pandu Kificho.
Bunge Maalumu la Katiba lililoanza Februari 18, mwaka huu, limeendelea kuonyesha dalili za kuwa na hatima mbaya katika safari yake, inayokusudia kujadili na hatimaye kupitisha Rasimu ya Katiba ya Mwaka 2013, iliyotolewa na Tume ya Mabadiliko ya Katiba.
Hiyo ni kutokana na hofu itokanayo na kuwapo kwa kila dalili kwamba Bunge hilo linaweza lisifikie lengo kuu ambalo ni kuipitisha rasimu hiyo baada ya kuijadili.

Rasimu hiyo imepangwa kuwasilishwa na Mwenyekiti wa Tume hiyo, Jaji Joseph Warioba, baada ya Rais Jakaya Kikwete, kulizindua Bunge hilo, pamoja na makatibu, mwenyekiti na wajumbe wake kuapishwa.

Kinyume cha mwongozo na wosia uliowahi kutolewa na Rais Kikwete wakati yeye na Rais wa Zanzibar, Dk. Ali Mohammed Shein, wakikabidhiwa rasimu hiyo na Tume ya Mabadiliko ya Katiba, hivi sasa wajumbe wa Bunge hilo wamegawanyika katika makundi makubwa mawili hasimu.

Kundi la kwanza, linaongozwa na Chama Cha Mapinduzi (CCM) kupitia wajumbe, ambao ni wanachama wake waliomo kwenye Bunge hilo.

La pili, linaundwa na wajumbe kutoka vyama vya upinzani, baadhi ya wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Baraza la Wawakilishi la Zanzibar, baadhi ya mashirika yasiyokuwa ya kiserikali na taasisi za kidini.

Mvutano baina ya makundi hayo mawili, umedhihirika wakati wa mjadala wa Rasimu ya Kanuni za Bunge Maalumu za Mwaka 2014.

Mjadala huo ulifanyika kupitia semina iliyotolewa kwa wajumbe hao bungeni, Jumatano na Alhamisi, wiki iliyopita.

Pamoja na mambo mengine, mgawanyiko mkubwa baina ya wajumbe hao unatokana na ibara ya 37 kifungu cha (3) na cha (4) vya rasimu ya kanuni hizo.

Vifungu hivyo vinapendekeza utaratibu utakaotumiwa na Bunge Maalumu kupata uamuzi katika vikao vyake.

Katika utaratibu huo, vifungu hivyo vinapendekeza kuwa baada ya Mwenyekiti wa Bunge Maalumu kutoa swali la kulihoji Bunge, itapigwa kura ya siri, ambayo itaitwa “kura ya mwisho.”

Vifungu hivyo vinaeleza: “Kwa madhumuni ya Kanuni hii, utaratibu utakaotumika kupata uamuzi baada ya Mwenyekiti wa Bunge Maalumu kutoa swali la kulihoji Bunge Maalumu utakuwa ni wa kura ya siri.”

“Bila kuathiri masharti ya Sheria na Kanuni hizi, wakati wa kupata uamuzi Bunge Maalumu kuhusu kupitisha Rasimu ya Katiba, Bunge Maalumu litapiga kura ya siri, ambayo kwa madhumuni ya Kanuni hii, itaitwa “kura ya mwisho.”

Kundi la kwanza la wajumbe, wengi wakiwa ni wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wajumbe wa Baraza la Wawakilishi la Zanzibar kutoka CCM, baadhi ya viongozi wa dini na makundi ya kijamii, wanataka utaratibu utakaotumiwa na Bunge Maalumu kupata uamuzi uwe wa kura za wazi.

Kundi la pili, linaloongozwa na vigogo wa vyama vya upinzani, wajumbe wengi kutoka makundi ya kijamii na baadhi ya viongozi wa dini na wabunge wa Bunge la Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, wakiwamo wachache wa CCM, wanataka utaratibu utakaotumiwa uwe wa kura za siri.

Hoja ni nyingi zinazotolewa na kundi la kwanza kushikilia msimamo wake wa kura ya wazi.

Lakini kubwa ni kwamba, wanadai kuwa utaratibu wa kura ya wazi utawawezesha wajumbe wa Bunge Maalumu la Katiba kuwaonyesha watu wanaowawakilisha nini wameamua bungeni yaliyomo kwenye Rasimu ya Katiba.

Kundi hilo linadai kuwa utaratibu wa kura ya siri katika kuamua kuhusu kitu kama katiba ni wa woga na una mbaya kutaka kuficha nia ovu ya rushwa.

Kundi la pili, nalo pia lina hoja nyingi linazoziona kuwa ni halali kung’ang’ania msimamo wake wa kutaka utaratibu wa kupata uamuzi kwa kupiga kura ya siri.

Kubwa ni kwamba, linadai kuwa utaratibu wa kura ya siri ni wa kidemokrasia na pia unazingatia uhuru wa mtu, haki za binadamu na unalinda usalama wa mtu dhidi ya vitisho, ambavyo anaweza kuvipata kutoka kwa viongozi wake iwapo watatofautiana katika misimamo na maamuzi.

Vilevile, wanadai kuwa ni utaratibu unaotumika pia katika kuchagua viongozi wa kisiasa, kama vile mwenyekiti wa serikali ya mtaa, diwani, mbunge na hata rais.
Mbali na kauli ya kamati ya kanuni iliyoongozwa na Profesa Costa Mahalu, kwamba hoja za kila upande zina misingi wa kidemokrasia, hali bado ni tete baina ya makundi hayo mawili ya wajumbe wa Bunge hilo. 
Pamoja na mambo mengine, kubwa ni kwamba, hali hiyo inaonekana kuwa inatokana na kila upande kushikilia msimamo wake na kutokuwa tayari kuridhia msimamo wa mwingine.

Hapo ndipo pia wengi wanaposhindwa kuelewa mantiki ya ushauri uliotolewa na kamati ya kanuni kwamba, utaratibu utakaotumiwa na Bunge Maalumu kufanya uamuzi, uamuliwe na wajumbe wenyewe!

Hawa tayari wana ukinzani mkubwa huku kila siku wakiingia bungeni, kazi ni kubishana na kuvutana! Hilo wanalorejeshewa waliamue ndilo la kuja kuwaongoza baadaye, linawagawa.

Je, watawezaje kulitatua wenyewe? Na walitatue kwa utaratibu gani, ambao utaridhiwa na kila kundi?

Ni dhahiri kuwa kila anayefuatilia mvutano huo, ana wasiwasi mkubwa juu ya uwezekano wa hali hiyo kuzifanya pande mbili hizo kutofikia suluhu.

Tayari wabunge wa CCM wameshakutana mara mbili kupeana mikakati na kujipanga namna ya kushiriki vikao vya Bunge hilo.

Upande mwingine, wajumbe wengine wa Bunge hilo, wakiongozwa na baadhi ya vigogo wa vyama vya upinzani nchini, wameunda Umoja wa Katiba ya Wananchi (Ukawa).

Mjumbe wa Ukawa, Profesa Ibrahim Lipumba, anasema lengo la kuunda umoja huo ni kukabiliana na njama zozote za rasimu ya katiba kuchakachuliwa katika Bunge hilo.

Yote tisa. Lakini kumi, sababu kubwa ya mvutano huo ni muundo wa Muungano. Kundi moja linataka uwe wa serikali tatu, kama inavyopendekezwa kwenye Rasimu ya Katiba na mwingine unataka uwe wa serikali mbili.

Pengine suala hilo pamoja na mambo mengine yaliyomo kwenye Rasimu ya Katiba ndiyo yaliyomfanya Rais Kikwete kushtuka na siku aliyokabidhiwa rasmi ya Pili aliwataka wajumbe kujadiliana na kukubaliana bungeni vingine watashindwa kupata Katiba Mpya inayopendekezwa.

Itakumbukwa namna alivyowahi kuwasihi wajumbe watakaojaliwa kuingia kwenye Bunge hilo kutumia busara kikamilifu wakati wa kuijadili Rasimu ya Katiba ili matunda yanayotarajiwa na wananchi yapatikane kwa ajili ya Watanzania wote na siyo watu au kikundi fulani cha watu au taasisi fulani.

Rais Kikwete alisema dhamana ya Tanzania na Watanzania ipo mikononi mwa wajumbe hao, hivyo akawasihi wawe makini kwa kutambua nini Watanzania wanahitaji, badala ya kuweka mbele maslahi yao, itikadi, mapenzi na ushabiki wa kimakundi.

Kwa uchache, alisema iwapo watafanya mchezo, mbali na kukosa katiba nzuri, watakosa katiba mpya kabisa.

Kwa mvutano uliopo baina makundi hayo mawili, ni wazi kuwa sasa naanza kumuelewa Rais Kikwete. Kwamba, aliona mbali na dalili za kutofikiwa kwa suluhu katika Bunge hilo zinaanza kuonekana.

Kinachoonekana ni wajumbe kutunishiana misuli ya kiitikadi, huku wakisahau kuwa wanachojadili ni hatima ya nchi.

Hawataki kabisa kuweka vyama vyao kisogoni na kuweka nchi kwenye paji la uso wakati wa mijadala yao.

Iwapo hali hii itaendelea na wajumbe hawatotumia busara, ni wazi kuwa hata wakiongezewa mwaka, kamwe suluhu haiwezi kupatikana.

Na iwapo suluhu itakosekana, wajue kuwa wananchi watachoka, wataandamana kumuomba Rais asilizindue Bunge hilo.

Kwani wananchi wana mahitaji mengi. Iweje yatumike mabilioni ya shilingi kwa Bunge ambalo halina tija?

Maana kuna hatari mvutano unaoendelea wa rasimu ya kanuni za Bunge Maalumu ‘kutafuna’ hizo siku 70 za Bunge hilo huku zikiendelea kutetketeza mabilioni ya shilingi za walipakodi, huku suluhu ikikosekana.

Kwa sababu wataendelea kubishana tu kila siku, huku wakiwa hawana kanuni zinazowaongoza wala kuapishwa.
 
CHANZO: NIPASHE