Sunday, July 21, 2013

Ni Vilio ...vilio

Ni baada ya miili saba ya wanajeshi waliouawa Darfur kuwasili Dar
Kuagwa kesho...kila mpiganaji aliyeuawa atafidiwa sh. milioni 113

 
Askari wa Jeshi la Wananchi wa Tanzania wakiwa wamebeba moja ya majeneza saba yaliyobeba miili ya wanajeshi waliokuwa katika kikosi cha Umoja wa 
 
Mataifa cha walinda amani wa Darfur nchini Sudan.
Vilio na mayowe jana vilitawala Uwanja wa Ndege wa Kimataifa wa Mwalimu J.K Nyerere jijini, Dar es Salaam, wakati miili ya askari saba wa Jeshi la Wananchi Tanzania (JWTZ) ilipowasili kutoka Dafur nchini Sudan.

Askari hao waliuawa Jumamosi iliyopita kwenye shambulizi la kushtukiza, huku wengine kujeruhiwa.
Ndugu wa marehemu wakiwemo watoto, wake zao na marafiki walikuwa wakilia wakati wote tangu miili hiyo ilipowasili uwanjani hapo na kushukia Terminal 1-Air wing (kikosi cha anga).

Baadhi ya jamaa za marehemu walishindwa kuzungumza , wengine wakishikiliwa kuwazuia wasianguke kutokana na huzuni ya msiba huo.
Ndege maalum ya Umoja wa Mataifa (UN) yenye namba B 737- 400 COMBI, ilileta miili hiyo na kutua uwanjani hapo saa 10:45 jioni.

Miili hiyo iliondolewa na kuingizwa katika magari  saba ya JWTZ kila mmoja ukisafirishwa peke yake kwenye msafara ulioongozwa na pikipiki za jeshi na kupelekwa Hospitali ya Jeshi Lugalo.

Makamu wa Rais Dk. Mohamed Gharib Bilal, aliwaongoza viongozi wa serikali akiwamo Mkuu wa Majeshi ya Ulinzi, Jenerali Davis Mwamunyange, pamoja na mamia ya wananchi waliofika uwanjani kuwapokea marehemu hao.

Naye Kaimu Mkurugenzi wa Habari wa JWTZ, Meja Joseph Masanja, alisema marehemu wataagwa kesho saa 2:30 asubuhi katika viwanja vya Wizara ya Ulinzi na Jeshi la Kujenga Taifa, Upanga jijini.

Alisema miili hiyo itaagwa kwa heshima zote za kijeshi na baadaye kusafirishwa kwa ajili ya mazishi.

Akizungumza uwanjani hapo, msemaji wa familia ya Sajenti Shaibu Othumani, alisema wamepata pigo kubwa kwa kuwa ndugu yao alikuwa tegemeo katika familia hiyo.

Shemeji wa marehemu Othuman aliyejitaja kwa jina la Rehema akizungumza huku akiwa analia alisema wamepatwa na majonzi na kwamba ni vigumu kumsahau mtu waliyetoka naye mbali.

Wanajeshi hao ni Sajenti Othuman , makoplo Oswalid Chacha, Mohamed Juma na Mohamed Chukilizo. Wengine ni maprivate Rodney Ndunguru , Peter Werema na Fortunatus Msoffe.

FIDIA KWA MAREHEMU
Kila mpiganaji aliyeuawa atafidiwa Dola za Marekani 70,000 ( karibu Sh. milioni 113) kwa mujibu wa viwango vya Umoja wa Mataifa (UN).

Fedha hizo zimetajwa na vyombo vya habari vya kigeni kuwa ni kiwango kinachotolewa na UN kwa askari anayeuawa akiwa kwenye operesheni za kulinda amani zinazosimamiwa na chombo hicho.

Wapiganaji saba kati ya 14 wa JWTZ walioko Dafur kwenye kikosi cha kulinda amani kinachoundwa na UN pamoja na Umoja wa Afrika (Unamid), Jumamosi iliyopita waliuawa baada ya kushambuliwa kwenye tukio la kushtukiza.

Chini ya utaratibu wa UN wa fidia, kila mpiganaji aliyepoteza maisha atafidiwa Dola 70,000 kwa mujibu wa taarifa za Radio Sauti ya Ujerumani (DW) Idhaa ya Kiswahili, zilizotangazwa jana asubuhi.

DW ilifanya mahojiano na Kaimu Msemaji wa Kurugenzi ya Mawasiliano ya JW, Meja Joseph Masanja na kumhoji kuhusu fidia hiyo kutolewa kwa jamaa waliopoteza ndugu zao .

Akijibu Kaimu Msemaji wa JW alisisitiza kuwa fidia ya marehemu hao itakuwepo lakini hakupinga kiwango cha (UN) wala kukubali badala yake alisema kinachofanyika kwa wakati huu ni kuwaleta marehemu hao nchini na kuwafikisha sehemu ambazo jamaa zao wamezitayarisha kwa ajili ya kuwazika.

Kama familia hizo zitafidiwa kiasi hicho, kila aliyepoteza jamaa yake atapokea zaidi ya Sh milioni 100 bila kuhusisha fidia kwa taifa. (Dola ni karibu Sh 1,620).

Katika mahojiano hayo, Kaimu Msemaji wa JWTZ aliulizwa iwapo serikali ina mpango wa kuwafidia askari hao, hata hivyo alikwepa kujibu swali hilo na kuzungumzia zaidi juu ya kuwapokea na kuwazika.
 
CHANZO: NIPASHE JUMAPILI

No comments:

Post a Comment